Beef kati ya T.I. na 50 Cent imeingia hatua mpya baada ya mtoto wa T.I., King Harris, kumtukana vikali 50 Cent kufuatia hatua ya rapa huyo kumdhalilisha mama yake, Tameka “Tiny” Harris, kwenye Instagram.
Chanzo cha mgogoro huu ni sakata la VERZUZ ambalo liliwahi kuzungumzwa kwa miaka kadhaa. T.I. hivi karibuni alifunguka kwenye kipindi cha Million Dollaz Worth of Game akisema kuwa heshima yake kwa 50 Cent ilipotea baada ya kile alichodai ni tabia ya “kukwepa makubaliano.”
Kwa mujibu wa T.I., wawili hao waliwahi kukubaliana faraghani kuhusu kufanya pambano la muziki la VERZUZ kama njia ya kusherehekea catalogue zao. Mpango ulikuwa T.I. atalitaja wazo hilo hadharani kisha 50 ajibu. Lakini baada ya T.I. kulizungumzia, 50 alidaiwa kujifanya hajui chochote.
Hata hivyo, mambo yalichafuka zaidi pale 50 Cent alipoweka picha ya Tiny kwa mtazamo wa kumdhalilisha, akiandika: “I keep saying keep my name out ya mouth.” Kitendo hicho kilimkera King Harris, ambaye alirekodi video kali ya kumjibu 50 Cent.
Katika video hiyo, King ametoa maneno makali akimtaka 50 aache kumtaja mama yake na kuonesha heshima.
Alimshambulia kwa maneno ya kuudhi, akisema hatokubali mama yake kudhalilishwa na akamwambia 50 “aweke maua kaburini kwa mama yake” badala ya kuchezea jina la Tiny.
Video hiyo imezua mjadala mkubwa mitandaoni, huku mashabiki wakigawanyika. Wengine wanaona King amechukua hatua kulinda heshima ya mama yake huku wengine wakimuonya kwa hatari ya kuingia vitani na 50 Cent.
