Gianni Infantino amesema wachezaji wanaofunika midomo kwa jezi zao wanapozungumza uwanjani wanaweza kupewa kadi nyekundu iwapo watabainika kutoa kauli za kibaguzi. Kauli hiyo imekuja kufuatia tukio lililomhusisha Vinícius Júnior wa Real Madrid CF na Gianluca Prestianni wa SL Benfica, ambapo Prestianni alituhumiwa kumtolea Vinicius kauli ya kibaguzi huku akifunika mdomo wake, madai aliyoyakanusha akisema alitoa tusi la ushoga.

UEFA imeanzisha uchunguzi kuhusu tukio hilo na Prestianni amesimamishwa kwa muda wakati uchunguzi ukiendelea. Infantino aliiambia Sky News kuwa mchezaji anayefunika mdomo wake anapaswa kubeba dhamana ya maneno yake, akisisitiza kuwa kama hana jambo la kuficha, hana sababu ya kujifunika anapozungumza. Amesema hatua kali ni muhimu kuonyesha uzito wa mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi.
Ripoti zinaeleza kuwa pendekezo la kuadhibu tabia hiyo bado liko katika hatua za awali za majadiliano, bila utekelezaji wa haraka. Hata hivyo, limepata uungwaji mkono kutoka baadhi ya vyama vya soka vya England vilivyo ndani ya IFAB pamoja na FIFA. Wakati huohuo, kocha wa Benfica, José Mourinho, amesema iwapo mchezaji wake atapatikana na hatia ya ubaguzi, hatavumilia na mustakabali wake ndani ya timu utakuwa mashakani.
