
Mkuu wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW), Profesa Philipo Sanga, ameeleza kuwa idadi ya Watanzania wanaojua kusoma na kuandika imefikia asilimia 83.
Profesa Sanga ametoa kauli hiyo mkoani Katavi wakati akizungumza na waandishi wa habari katika maadhimisho ya Juma la Elimu ya Watu Wazima.
Ameutaja Mkoa wa Katavi kuwa ni miongoni mwa mikoa yenye idadi kubwa ya watu wasiojua kusoma na kuandika, kwa asilimia 29.6, ambapo mikoa mingine ni Tabora, Rukwa, Dodoma na Simiyu.
Profesa Sanga ameeleza kuwa mikakati ya taasisi hiyo ni kuhakikisha kuwa idadi ya watu wasiojua kusoma na kuandika inapungua na hatimaye kumalizika kabisa, pamoja na kuendana na kasi ya ukuaji wa sayansi na teknolojia.
Maadhimisho ya Kisomo Duniani na Juma la Elimu ya Watu Wazima mwaka 2025 yamebeba kauli mbiu isemayo “Kukuza kisomo katika zama za kidigitali kwa maendeleo endelevu ya Taifa letu”.