Mshambualiaji Mohamed Salah (33), leo Jumanne ametangaza rasmi kuwa ataachana na Liverpool baada ya msimu huu kumalizika.
Baada ya kuitumikia Liverpool kwa zaidi ya miaka nane tangu alipojiunga nayo 2017 akitokea AS Roma, Salah ambaye pia ni nahodha wa Misri, ametumia kurasa zake za mitandao ya kijamii kuaga klabuni hapo.
“Hallo kila moja. Hatimaye siku imefika. Hii ni sehemu ya kwanza ya kuaga kwangu. Nitaondoka Liverpool mwishoni mwa msimu.
“Nilitaka kuanza kwa kusema kwamba sikuwahi kufikiria jinsi klabu hii, jiji hili, na watu hawa wangekuwa sehemu muhimu sana ya maisha yangu.
“Liverpool si klabu ya mpira wa miguu tu. Ni shauku, ni historia, ni roho ambayo siwezi kuielezea kwa maneno,” amesema Salah.
Baada ya Salah kutoa taarifa hiyo, Liverpool imesema kuwa mchezaji huyo ataagwa kwa heshima mwishoni mwa msimu na sio sasa.

“Salah alieleza nia yake ya kutoa tangazo hili kwa mashabiki mapema iwezekanavyo ili kuweka wazi mustakabali wake, kutokana na heshima na shukrani alizonazo kwao.
“Bado kuna mengi ya kupigania msimu huu, hivyo Salah ameweka mkazo wake wote katika kuhakikisha anapata matokeo bora iwezekanavyo kwa Liverpool. Kwa hiyo, muda wa kusherehekea kikamilifu urithi na mafanikio yake utafika baadaye mwaka huu atakapoiaga Anfield,” imesema taarifa ya Liverpool.
Salah katika kipindi chote alichoitumikia Liverpool, amecheza idadi ya mechi 435, akifunga mabao 255 na kupiga pasi za mwisho 122.
Ameshinda mataji nane akiwa na Liverpool ambayo ni moja ni la Klabu Bingwa ya Dunia, moja la Ligi ya Mabingwa Ulaya, moja la UEFA Super Cup, mawili ya Ligi Kuu England, moja la FA, moja la Carabao na moja la Ngao ya Jamii England.
Anahusishwa kujiunga na Al Ittihad inayoshiriki Ligi Kuu ya Saudi Arabia.
