
Wizara ya Sheria ya Marekani imewafungulia mashtaka raia wake wanne kwa kuhusika kwao katika jaribio la mapinduzi dhidi ya serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), baada ya watatu kati yao kurejeshwa mikononi mwa mamlaka za Marekani wiki hii.
Marcel Malanga, Tyler Thompson, na Benjamin Zalman-Polun walikuwa tayari wamehukumiwa nchini DRC kwa kuhusika katika jaribio hilo lililoshindwa la mapinduzi lililotokea Mei 2024.
Imeelezwa kuwa watu waliokuwa na silaha walivamia makazi ya maafisa waandamizi wa serikali ya DRC na kwa muda mfupi walikalia ofisi ya urais jijini Kinshasa.
Watatu hao waliachiliwa huru siku ya Jumanne katika makubaliano yaliyofikiwa wakati wa ziara ya mshauri mkuu wa Rais wa Marekani Donald Trump kuhusu masuala ya Afrika, Massad Boulos, nchini DRC.
Kwa mujibu wa taarifa rasmi, watuhumiwa wanakabiliwa na mashtaka ya kula njama ya kutumia silaha za maangamizi, kulipua majengo ya serikali, na kupanga kuua au kuwateka nyara watu katika nchi ya kigeni.